Saturday, November 12, 2011

WAHISANI WAOMBWA KUSAIDIA KUBORESHA KILIMO TANZANIA.

RAIS Jakaya Kikwete amewataka wahisani kuendelea kusaidia sekta ya kilimo nchini ili kufikia asilimia 10 ya pato la taifa.Alitoa wito huo jana jijini Dar es Salaam alipokuwa akifungua mkutano wa siku mbili wa Mpango wa Uwekezaji katika Kilimo na Uhakika wa Chakula (TAFSIP) wa mwaka 2011/12 mpaka 2020/2021.

Rais Kikwete alisema kilimo kitafanikiwa kutokana na misaada ya wahisani hao, sekta binafsi na vyama vya kijamii vinapaswa kusaidia sekta ili kufikia malengo yake.

"Malengo ni kufikia asilimia 10, sasa tuko kwenye asilimia 4, hivyo pato la taifa likifikia asilimia 10, tutakuwa tumefika mbali,"alisema Rais Kikwete.

Alisema endapo mpango huo utafanikiwa, wakulima wengi nchini wataondokana na umasikini na uchumi wan chi kukua.

"Uchumi wetu unakuwa vizuri na sasa umekua kwa asilimia 7 hivyo kama tutafanikiwa kukuza kilimo na kufikia asilimia 10 ya pato la taifa, basi nao uchumi utafikia asilimia 10 katika sekta zote.


"Kilimo ndicho kinachotoa chakula na pia kinaingiza fedha za kigeni.

"Japokuwa hakijakuwa kama tulivyotegemea, nia hasa ni kuhakikisha kilimo kinakuwa,"alisema.

Balozi wa Marekani nchini Tanzania, Alfonso Lenhardt alisema nchi yake itaendelea kuisaidia Tanzania ili sekta ya kilimo ikue kwa kasi na kuwapo kwa uhakika wa chakula nchini.

"Tutasaidia mpango huo ambao unatekelezwa pande zote mbili za Tanzania Bara na Visiwani,"alisema Balozi Lenhardt.
Chanzo: Mwananchi

Monday, November 7, 2011

Wataalamu wa kilimo msikae ofisini

PICHANI : Mh. Leonidas Gama akiwa na Waziri wa nchi OWM -TAMISEMI Mheshimiwa Kapteni Mstaafu George Mkuchika (Katikati)

MKUU wa Mkoa wa Kilimanjaro Bw. Leonidas Gama, amewataka wataalamu wa Kilimo mkoani humo, kuacha tabia ya kukaa ofisini badala yake waende kwa wakulima kuwapa utalamu ili waweze kujikomboa katika lindi la umaskini kupitia sekta hiyo.
Bw. Gama aliyasema hayo mwishoni mwa wiki wakati akizungumza na viongozi mbalimbali wakiwemo Wakuu wa Wilaya, Makatibu Tawala, Wakurugenzi wa Halmashauri na wataalamu wa idara mbalimbali katika majumuisho ya ziara yake mkoani humo.

Alisema wataalamu wa kilimo na ufugaji hawana utamaduni wa kuwatembelea wakulima badala yake wanakaa ofisini hali ambayo inasababisha wakulima kujihusisha na kilimo cha mazoea.

“Hali ya kilimo katika Mkoa huu si mbaya sana lakini hali hii si kwamba inatokana na juhudi za wataalamu wetu wa kilimo hapana bali ni kutokana na wananchi wenyewe.

“Naomba kuanzia sasa, muende kwa wakulima ili waweze kulima kitaalamu na kupata mazao mengi hivyo kujikwamua kiuchumi,” alisema Bw. Gama.

Akizungumzia hali ya ufugaji mkoani humo, Bw. Gama alisema wananchi bado hawajanufaika na ufugaji kwani zipo changamoto nyingi ambazo zinaelezwa na wafugaji ikiwemo ukosefu wa chakula na ardhi ya malisho hali ambayo inasababishwa na wataalamu katika sekta hiyo kukaa ofisini.

Alisema wastani wa uzalishaji maziwa mkoani humo ni kati ya lita sita hadi nane ambao ni mdogo mdogo ukilinganisha nahali halisi ya mahitaji kwani wataalamu hao, wameshindwa kutoa mbinu mpya za ufugaji wa kitaalamu.

“Inaonesha kabisa wataalamu wetu wanakaa ofisini, hawaendi kwa wananchi kuwapa utaalamu, lazima wabadilike ili tuweze kuwakomboa wananchi na umaskini,” alisema

Alisema wataalamu hao wanapaswa kwenda kwa wananchi ili kutatua matatizo yao pamoja na kuwapa mbinu za kitaalamu juu ya kilimo na ufugaji ambazo zitawawezesha kufuga mifugo michache na kupata faida kubwa badala ya kufuga mifugo mingi wakati hakuna eneo la malisho.